Maelfu wahudhuria mazishi ya Waziri Mkuu wa kwanza wa Singapore Lee Kuan Yew
Maelfu ya wananchi wa Singapore wamejitokeza kuhudhuria ibada ya mazishi ya mwanzilishi wa taifa lao Lee Kuan Yew aliyefariki dunia siku ya Jumatatu juma hili akiwa na umri wa miaka 91.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Mvua kubwa inayonyesha haikuwazuia wananchi wa taifa hilo ambao juma hili wamekuwa wakitoa heshima zao za mwisho kwa kiongozi wao katika majengo ya bunge.
Wakati wa uhai wake, Lee alikuwa na uhusiano mzuri na viongozi wa nchi za Magharibi na amejizolea sifa nyingi kwa kuibadilisha Singapore kutoka nchi maskini hadi mojawapo ya nchi tajiri duniani.
Lee alikuwa Waziri Mkuu kwa miaka 31 na kujiuzulu mwaka 1990 lakini alisalia kuwa na ushawishi mkubwa ndani na nje ya nchi hiyo.
Alisaidia nchi yake kupata uhuru kutoka kwa wakoloni Uingereza na nchi yake kujitenga na Malaysia pamoja na kubadilisha maisha ya wananchi wa kawaida waliokuwa wanaishi kwa umasikini mkubwa.
Mwanye wa kwanza wa kiume ambaye pia ni Waziri Mkuu wa sasa Lee Hsien Loong amemwelezea babake kama mtu aliyetoa mchango mkubwa sana kwa wananchi wa Singapore wakati wa uhai wake.
Miongoni mwa viongozi wa kigeni waliofika kuhudhuria mazishi hauo ni pamoja na rais wa zamani wa Marekani Bill Clinton, Waziri Mkuu wa India Narendra Modi, Waziri Mkuu wa Australia Tonny Abbot na meenzake wa Japan Shinzo Abe.
Mwili wa Lee ulitembezwa katika mitaa ya jiji la Singapore na kuzikwa katika makaazi yake binafsi.