Kesi ya ung'atuzi dhidi ya Trump: Mahojiano ya wazi kuanza
Mahojiano ya wazi yanaanza leo Jumatano katika uchunguzi ambao unaweza kushuhudia rais Donald Trump akiondolewa madarakani. Mahojiano ambayo yatarushwa moja kwa moja kwenye televisheni.
Imechapishwa:
Taarifa ya wabunge wa chama cha Democrats imeonesha kuwa maofisa watatu wajuu kutoka wizara ya mambo ya nje wanatarajia kutatoa ushahidi, baada ya kuwa wamehojiwa kwa siri kwa majuma kadhaa.
Uchunguzi uliofanywa na wabunge ulijikita katika madai kuwa rais Trump alimshinikiza rais wa Ukraine kutangaza hadharani kuanza uchunguzi dhidi ya mpinzani wake Joe Biden.
Hivi karibuni mwenyekiti wa kamati ya Intelijensia, Adam Schiff ambaye anasimamia mchakato huu, amliwaambia waandishi wa habari kuwa taratibu zote zimekamilika ambapo pia wamechapisha nyaraka za mahojiano waliyofanya na mashahidi watakaoitwa.
Rais Trump kwa upande wake amekosoa mchakato huu ulioanzishwa na Wabunge wa Democrats akisema hakuna kosa alilofanya wakati wa maongezi yake na rais wa Ukraine, kauli anayoungwa mkono na baadhi ya wabunge wa chama chake.