Kiongozi wa upinzani Venezuela apokelewa na umati wa watu na mabalozi
Kiongozi wa upinzani nchini Venezuela Juan Guaido amerejea nchini, baada ya ziara katika mataifa ya Amerika, na kushinikiza maandamano zaidi dhidi ya rais Nicolas Maduro.
Imechapishwa:
Guaido ambaye alijiapisha kuwa rais wa watu na kuungwa mkono na mataifa ya Magharibi, yakiongozwa na Marekani, amepokelewa na maelfu ya wafuasi wake jijini Caracas.
Kiongozi huyo amerejea nyumbani licha ya wasiwasi kuwa angekamatwa, baada ya kukiuka masharti ya Mahakama ya Juu, iliyokuwa imemzuia kutoka nje ya nchi hiyo.
Guaido ameongeza kuwa, tumaini bado lipo na harakati zitaendelea ili kuhakikisha kuwa, rais Maduro anaondoka madarakani.
Kuendeleza shinikizo kwa rais Maduro, maandamano makubwa yanatarajiwa kufanyika siku ya Jumamosi, kuendelea kushinikiza kujiuzulu kwa rais Maduro na kumtaka kuitisha uchaguzi mpya.