Marekani yataka UNSC kushinikiza utawala wa Maduro
Nchi ya Marekani imesema italitaka Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kupitisha azimio kuhusu nchi ya Venezuela kushinikiza Serikali ya rais Nicolas Maduro kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingia nchini humo.
Imechapishwa:
Hatua ya Marekani imekuja saa chache tu baada ya utawala wa Washington kumshtumu rais Maduro na kumuita kama mla rushwa na mtawala wa kiimla ambaye yuko tayari kusalia madarakani kwa nguvu huku wananchi wakiteseka.
Mjumbe maalumu wa rais Donald Trump kwa nchi ya Venezuela, Elliott Abrams amesema Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linatarajiwa kupiga kura juma hili kupitisha mapendekezo yake, ingawa ni wazi azimio hilo litakutana na upinzani kutoka kwa serikali ya China na Urusi.
Haya yanajiri wakati huu kukiripotiwa kuwa zaidi ya wanajeshi 300 wameasi jeshi la nchi hiyo na kukimbilia kwenye nchi jirani ya Colombia na Brazil.
Rais Maduro mwenyewe anaituhumu Marekani na mataifa ya Ulaya kwa kujaribu kutumia kigezo cha misaada kuivamia nchi yake.