Marekani yatishia kujiondoa katika Shirika la Biashara Duniani WTO
Rais wa Marekani Donald Trump ametishia kuindoa nchi yake katika Shirika la Biashara Duniani WTO “kama hakutakua na mabadiliko katika utendaji wa shirika hilo kwa Marekani”.
Imechapishwa:
Rais Donald Trump ametoa kauli hiyo alipokua akihojiwa na Jarida la Bloomberg , huku akibaini kwamba iwapo WTO halitajirekebisha hatosita kuiondoa nchi yake katika shirika hilo.
Shirika hilo la Biashara Duniani lilianzishwa kwa ajili ya kusimamia sheria za biashara duniani na kutatua tofauti kati ya nchi.
Hali hii inaonyesha kuwepo kwa mvutano katika Shirika la Biashara Duniani (WTO)kufuatia sera za kibiashara za Rais Donald Trump na mfumo wa biashara huru ambao shirika hilo unasimamia.
Si mara ya kwanza Marekani kukosoa utendaji wa WTO. Hivi karibuni Mwakilishi wa Markani katika masuala ya biashara Robert Lighthizer alishtumu shirika hili kwamba linaingilia mamlaka ya Marekani.
Haribuni Marekani ilipinga uchaguzi wa majaji wapya wa mfumo wa WTO wa kukabiliana na mashauri jambo ambalo linaweza kukwamisha uwezo na utaratibu wa kutoa hukumu.