Maduro: Bunge jipya la Katiba kuapishwa Ijumaa
Rais wa Venezuela Nicolas Maduro amesema bunge jipya lililochaguliwa hivi majuzi litaapishwa siku ya Ijumaa. Jeshi la polisi ambalo limekuwa likikabiliana na waandamanaji limeimarisha ulinzi kila mahali nchini humo.
Imechapishwa:
Maduro alitangaza kuahirishwa huko baada ya Upinzani kupanga maandamano makubwa hapo jana siku ya jumatano, ambapo ilitarajiwa kuwa bunge hilo jipya lingeapishwa.
Wabunge hawa wapya wanatarajiwa kuiandika katiba mpya, katika zoezi ambalo upinzani unasema ni mbinu iliyotumiwa na rais Nicolas Maduro kuchukua madaraka kwa nguvu.
Serikali ya Venezuela imeamuru kukamatwa kwa wakosoaji wakubwa wawili wa Maduro, hali ambayo imeongeza hasira ya wapinzani kuhusiana na kura iliyofanyika siku ya Jumapili, na kusababisha Marekani kuweka vikwazo dhidi ya rais huyo wa Venezuela.
Upinzani unataka kuachiliwa huru kwa baadhi ya viongozi wake lakini pia kupinga bunge hili. Msemaji wa halmashauri ya Umoja wa ulaya Catherine Ray amewaambia waandishi habari kwamba majadiliano yanaendelea.