Trump:Uvumilivu wa Marekani kwa Korea Kaskazini umefika mwisho
Rais wa Marekani Donald Trump ametangaza kuwa uvumilivu wa Marekani dhidi ya Korea ya Kaskazini na majaribio yake ya makombora umefika mwisho.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Trump ametoa kauli hiyo Jana Ijumaa wakati akimpokea rais mpya wa Korea Kusini Moon Jae-In kwa mazungumzo katika ikulu ya White House.
Wakati Moon akimtaka Trump kushirikiana kwa karibu na Pyongyang kama njia bora ya kulainisha mipango yake ya nyuklia , Trump ameweka wazi kuwa hashawishiki kufanya diplomasia na serikali ambayo anaishutumu kuwa haiheshimu maisha ya watu.
Na wakati Moon akitangazakuwa Trump amekubali ombi la kutembelea Seoul baadaye mwaka huu, viongozi hao wameshindwa kupanga mkakati wa ushirikiano wa aina yoyote kuhusu namna bora ya kushughulikia vitisho vinavyowekwa na uongozi wa Korea Kaskazini.
Utawala wa Trump umeendelea kuchukizwa na utawala wa kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un ambao imetekeleza maajaribio kadhaa ya makombora katika miezi ya hivi karibuni.
Aidha kumekuwa na hasira kubwa nchini Marekani baada ya mwanafunzi Otto Warmbier, aliyekuwa kizuizini nchini Korea Kaskazini kwa miezi 18 , kufariki dunia siku chache baada ya kuachiwa akiwa hana fahamu mwezi uliopita.