Mkwe wa rais Trump, Jared Kushner kuhojiwa na kamati ya bunge la seneti
Mkwe wa rais wa Marekani Donald Trump na mshauri wake wa karibu, Jared Kushner, atahojiwa kamati ya bunge la Seneti inayochunguza madai kuwa nchi ya Urusi iliingia uchaguzi wa urais wa mwaka jana, taarifa ya ikulu ya White Imesema.
Imechapishwa:
Kushner mwenye umri wa miaka 36, alikuwa mshauri wa karibu wa rais Trump kwenye mawasiliano na ushirikiano na mataifa ya nje wakati wa kempeni za uchaguzi wa mwaka jana na sasa anafanya kazi kama hiyo kwenye ikulu ya Marekani.
Kushner ndiye aliyeandaa mkutano kati ya raia Trump na waziri mkuu wa Japan, Shinzo Abe na rais wa Mexico Enrique Pena Nieto.
Hata hivyo kwa sasa mawasiliano yake na viongozi kadhaa wa Urusi ndio yanaonekana kumulikwa kwa darubini kali wakati huu kukiwa na tuhuma nyingi kuhusu uhusiano wa timu ya kampeni ya Trump na utawala wa Kremlin.
Rais Trump amelipeleka suala hili hata kwenye mtandao wak wa kijamii akisisitiza kuwa uhusiano wa Trump na Urusi ni uongo mkubwa, akiwataka wabunge hao kujikita kumchunguza mpinzani wake aliyeshindwa Hillary Clinton.
Mashirika ya ujasusi ya Marekani tayari yamesema wazi kuwa nchi ya Urusi ilikuwa na mtandao mpana wakati wa uchaguzi wa mwaka jana uliokuwa na lengo la kumsaidia Trump kushinda uchaguzi huo.
Ikulu ya Marekani inasema kuwa wakati wote wa kampeni na mabadilishano kati ya utawala wa Obama na Trump, Jared Kushner alikuwa kama sehemu ya mawasiliano makuu na Serikali za nje.
Na ni kutokana na mchango wake huu, ikulu ya Washington inasema ndio maana Kushner amekubali kwenda kuhojiwa na kamati ya bunge la Seneti.