WHO: Ebola yaendelea kuathiri raia wa DRC
Shirika la Afya Duniani (WHO) linasema linasubiri idhini kutoka kwa serikali ya DRC, ili kutuma dawa ambayo haijaidhinishwa kusaidia kupambana na ugonjwa hatari wa Ebola Kaskazini Magharibi mwa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Watu 54 wameambukizwa kwa kipindi cha wiki kadhaa zlizopita, huku 25 wakipoteza maisha.
Pamoja na dawa hii, tayari WHO inatumia chanjo ambayo pia haijaidhnishwa kuona iwapo itasaidia kuzuia kusambaa kwa ugonjwa huu hatari.
Awali shirika la Afya duniani (WHO) lilisema ugonjwa hatari wa Ebola haujafika kiwango cha kutangazwa hali ya dharura.
Katika mkutano huko Geneva ulioitishwa kwa dharura kujadili Ebola katika Jamhuri ya Kidmeokrasi ya Congo - shirika hilo limesema mlipuko wa sasa haijafikia vigezo vya kutangazwa hali ya hatari na halikupendekeza vizuizi vyovyote vya usafiri wala biashara.
Kamati ya muongozo wa kimataifa ya shirika hilo hatahivyo imesema kuna haja ya kuwa na wasiwasi kutokana na aina ya mlipuko wa sasa wa Ebola DRC.
Kumetokea milipuko kadhaa katika maeneo ya mashinani na maeneo ambayo sio rahisi kuyafikia.
WHO inasema imewatambua zaidi ya watu 500 ambao huenda walikaribiana na waathiriwa wa ugonjwa wa Ebola nchini Congo.
Mataifa jirani na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo yamekuwa katika hali ya tahadhari kubwa kuhakikisha wanadhibiti kuingia kwa virusi hivyo katika maeneo yao.