Zaidi ya watu 100,000 watoroka makazi yao kufuatia machafuko DRC
Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia wakimbizi (UNHCR) linasema lina wasiwasi mkubwa kuhusu hali inayozidi kuwa mbaya katika eneo la Beni, Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), watu wanaendelea kuyatoroka makazi yao.
Imechapishwa:
UNHCR limebaini kwamba ambapo machafuko katika Wilaya ya Beni yamesababisha zaidi ya watu 100,000 kuyatoroka makazi yaondani ya kipindi cha miezi miwili iliyopita.
Msemaji wa UNHCR, Andrewj Mahecic alisema hayo katika mkutano na waandishi wa habari huko Geneva.
Mashambulizi ya makundi yenye silaha tangu mwezi Desemba mwaka uliopita dhidi ya raia wa miji na vijiji katika eneo la Watalinga, karibu na mpaka na Uganda, yamesababisha wanawake, wanaume na watoto kuyatoroka makaazi yao na kuelekea mji wa Nobili na maeneo jirani, UNHCR imebaini.
Wengi wao walikuwa ni wakimbizi wa ndani na tayari walikuwa walirejea katika vijiji vyao mwezi Novemba 2019, baada ya kukimbia machafuko mwezi Aprili mwaka jana, kwa mujibu wa Radio Okapi.
"Raia, pamoja na wale waliotoroka makaazi yao mwezi Novemba na Desemba, ni miongoni mwa wanaolengwa na makundi yenye silaha, ikiwa ni pamoja na waasi wa Uganda wa ADF. Kulingana na viongozi wa eneo hilo, karibu watu 252 wameuawa katika eneo la Beni tangu Desemba 2019. Wengi wamewaambia wafanyakazi wa UNHCR kwamba sasa wanaishi kwa hofu, baada ya kushuhudia mauaji, unyanyasaji wa kijinsia na visa vya utekwaji nyara, " UNHCR imesema.