Mafuriko DRC: Msaada wachelewa kuwafikia walengwa
Raia walioathiriwa na mafuriko Kaskazini mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wanaendelea kusubiri kwa wiki tatu msaada kutoka serikali na mashirika ya kihisani nchini humo.
Imechapishwa:
Waziri wa Masuala ya Kibinadamu na Mshikamano wa Kitaifa, Steve Mbikayi, amesema makumi ya maelfu ya watu wameathiriwa na mafuriko hayo.
Mikoa mitatu sasa imeathiriwa na mafuriko ikiwa ni pamoja na Mongala, Ubangi Kaskazini na Ubangi Kusini, kulingana na vyanzo vya serikali.
Maji yanaendelea kuongezeka na mafuriko yameathiri miji mikubwa.
Maeneo mengi yamekumbwa na mafuriko na nyumba kadhaa zimeporomoka.
Katika mji mkuu wa Mkoa wa Ubangi Kaskazini, Gbadolite, maeneo ya Mogoro na Kambo yamekumbwa na mafuriko.
Katikati ya mji, maeneo kama Kaya au Mbanza pia yameathiriwa na mafuriko, huku nyumba kadhaa zikiporomoka. Barabara nyingi na madaraja vilijengwa katika utawala wa Mobutu.