Hamdok: Nataka kurejesha amani Darfur
Waziri Mkuu wa Sudan Abdallah Hamdok amewahakikishia Jumatatu wiki hii waathiriwa wa mgogoro wa Darfur kuwa serikali yake imeundwa kwa minajili ya kurejesha usalama na amani katika jimbo hilo.
Imechapishwa:
Bw Hamdok ameyasema hayo wakati wa ziara yake ya kwanza katika Jimbo la Darfur, Magharibi mwa Sudan.
Abdallah Hamdok anazuru Darfur katika ziara ya siku moja. Darfur ilikumbwa na mgogoro mnamo mwaka 2003 uliohusisha kundi la waasi lililodai kutengwa na utawala wa Rais Omar al-Bashir aliyeng'atuliwa madarakani.
Karibu watu 300,000 waliuawa na milioni 2.5 walilazimika kutoroka makaazi yao wakati wa mgogoro huo, kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa.
Waziri Mkuu amekutana na waathiriwa katika mji wa El-Facher, mji mkuu wa Darfur Kaskazini, ambapo kunapatikana kambi nyingi za mamia ya maelfu ya wakimbizi wa ndani wa Sudani kwa miaka kadhaa.
"Tunataka tutendewe haki! Watumeni wahalifu wote wa Darfur katika Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai (ICC)," wakimbizi wamekuwa wakiimba wakati wa zaiara ya Bw Hamdok katika kambi mbili za wakimbizi hao, mwandishi wa shirika la Habari la AFP amesema .
"Ninajua madai yenu," amesema Hamdok. "Sote tutashirikiana kutimiza maombi yenu na kuhakikisha maisha ya kawaida yanarudi," ameongeza, mbele ya umati wa watu waliokuwa wakiimba "hakuna haki, hakuna amani Darfur".