Pata taarifa kuu
DRC-MINEMBWE-USALAMA

DRC: Mauaji yaendelea Minembwe

Mashambulizi dhidi ya raia yanaendelea katika bonde la Ruzizi na Fizi, Katika Mkoa wa Kivu Kusini, Mashariki mwa Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

Kambi ya walinda amani kutoka Pakistani katikati mwa mji wa Minembwe, Oktoba 21, 2019.
Kambi ya walinda amani kutoka Pakistani katikati mwa mji wa Minembwe, Oktoba 21, 2019. © Sonia Rolley/RFI
Matangazo ya kibiashara

Katika mji wa Minembwe, hasa katika maeneo ya milimani, jeshi la DRC (FARDC) na kikosi cha Umoja wa Mataifa nchini humo, MONUSCO wameimarisha ngome zao lakini mauaji hayo yanaendelea.

Katika maeneo mbalimbali ya wilaya ya Minembwe, nyumba zimekuwa zikiteketea kwa moto. Mifugo, hasa Ng'ombe wametoweka. Wakaazi wengi walitoroka vijiji vyao na kukimbilia katikati mwa mji. Watu kutoka jamii ya Wanyamulenge ndi pekee wamesalia vijijini lakini Eli Ntambara, mwakilishi wa jamii hiyo, amesema hali hiyo isiambatanishwi mgogoro wa kikabila.

"Siku zote tumeishi mapoja na marafiki zetu, ndugu zetu. Kuna hata vijiji ambavyo jamii zote ziliishi pamoja. Lakini shida ni kwamba serikali haifanyi kazi kutokomeza makundi haya yenye silaha, " Eli Ntambara amesema.

Tangu mwezi Septemba mwaka huu, watu kutoka jamii zingine katika eneo la Minembwe walitoroka makaazi yao. Kuna wafanyabiashara wachache tu kutoka jamii ya Washi ambao wamebaki, lakini pia mwakilishi wa jamii ya Wafuliro.

Kwa upande wake Venance Kibingira, ameinyooshea kidole cha lawama serikali ya DRC akisema serikali inahusika kwa hali hii, lakini pia Rwanda na Burundi.

"Naweza hata kuthibitisha kwamba kuna watu wanaotumiwa kufanya hivyo. Kama hakungelikukuwa na hali hiyo, labda visa hivi vingelikuwa tayari vimekwisha. Lakini vinaendelea, kila wakati vinajirudia, na vinakwisha. Kwa hali hii, ninaweza kusema kuwa kuna nchi jirani ambazo zinatumiwa kuhatarisha usalama huu. Makundi yote yenye silaha yanayohatarisha usalama katika eneo hili yanatumiwa. Hakuna kundi hata moja ambalo halijatumiwa, "anasema Bw Kibingira.

Katika miezi ya hivi karibuni, makundi yenye silaha yanayoundwa na raia wa DRCyalihasimiana, lakini pia waasi kutoka Burundi na Rwanda.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya hii ya vijijini , Gady Mukiza, amesema kinachotokea Minembwe sio mgogoro wa kikabila. Kuna haja ya kuzindua oparesheni za kijeshi, amesema.

Tumeathiriwa sana na mashambulizi ya kila mara ya muungano wa makundi yenye silaha ya Mai-Mai [...] Walianza mwezi Machi na mkakati ambao haujaeleweka hadi wakati huu kwa kuteketeza nyumba kwa moto, na kuiba ng'ombe. Makundi ya waasi wa Burundi FNL na RED Tabara yanashirikiana na kundi la waasi wa DRC Mai-Mai [...] Sote tunapoteza, kwa sababu kila mtu anakimbia kwa kuhofia maisha yake, "Gady Mukiza, Mkuu wa wilaya Minembwe, akihojiwa na mwandishi wetu katika Maziwa Makuu, Sonia Rolley, amebaini .

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.