Mwanaharakati Alaa Abdel Fattah akamatwa tena Misri
Mwanaharakati nchini Misri Alaa Abdel Fattah, ambaye ni miongoni mwa viongozi wa maandamo dhidi ya rais wa zamani Hosni Mubarak Januari 2011 anazuiliwa tangu Jumapili (Septemba 29), familia yake na vyanzo vya mahakama wamebaini.
Imechapishwa:
Wakati alikuwa akitokea kituo cha polisi ambapo alilazimishwa kulala kila ifikapo usiku tangu kuachiliwa kwake huru Machi 29, Alaa Abdel Fattah "aliingizwa katika gari" na kupelekwa jela, familia yake imeongeza. Alaa Abdel Fattah alifungwa miaka mitano jela kwa "kushiriki katika maandamano haramu".
Tangu kuachiliwa kwake, Abdel Fattah alijizuia kufanya siasa, na kuridhika kutoa maoni yake katika masuala ya kijamii na kiuchumi kwenye mitandao ya kijamii. Abdel Fattah hakuitikia maandamano dhidi ya Rais Sissi siku ya Ijumaa hii na yale yaliyotangulia.
Wiki iliyopita, mwanaharakati mwingine na mmoja wa viongozi wa maandamano dhidi ya Mubarak, Mahienour el-Masry, alikamatwa.
Kwa mujibu wa mawakili wake, alishtakiwa kwa "kushirikiana na kundi la kigaidi [Muslim Brotherhood] na kusambaza habari za uwongo".