Pata taarifa kuu

Kiongozi wa waasi wa Kihutu wa Rwanda auawa mashariki mwa DRC

Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (FARDC) limetangaza kwamba "limemuangamiza kabisa" kiongozi mkuu wa kundi la waasi wa Kihutu wa Rwanda (FDLR), Sylvestre Mudacumura.

Wapiganaji wa FDLR katika kijiji cha Lushebere, mashariki mwa DRC, Novemba 2008.
Wapiganaji wa FDLR katika kijiji cha Lushebere, mashariki mwa DRC, Novemba 2008. © AFP PHOTO/ Tony KARUMBA
Matangazo ya kibiashara

Ikiwa taarifa hii itathibitishwa itakuwa ni pigo jingine kubwa kwa kundi la waasi wa Kihutu wa Rwanda, lenye makao yake makuu mashariki mwa DRC kwa miongo miwili sasa.

Msemaji wa jeshi la DRC, Jenerali Léon Richard Kasongo, amehakikisha kwamba kitengo maalum cha jeshi la DRC "kimemuangamiza kabisa" kiongozi mkuu wa kundi la waasi wa Kihutu wa Rwanda (FDLR), Sylvestre Mudacumura, usiku wa tarehe 17 kuamkia 18 Septemba, wakati wa operesheni iliyofanyika katika eneo la Bwito katika wilaya ya Rutshuru, katika mkoa wa Kivu-Kaskazini, mashariki mwa nchi.

Kwa mujibu wa msemaji wa FARDC, amesema kuuawa kwa kiongozi huyo wa kivita wa FDLR ni ushindi mkubwa kwa jeshi la DRC. Sylvestre Mudacumura aliuawa pamoja na maafisa wake kadhaa, kwa mujibu wa jeshi la DRC.

Léon Richard Kasongo hakutoa maelezo zaidi kuhusu operesheni hiyo ya kijeshi na amekanusha habari inayozunguka kwenye mitandao ya kijamii inayodai kwamba wanamgambo wa Jenerali Gédéon ndio waliomuua Sylvestre Mudacumura na maafisa wake.

Sylvestre Mudacumura na wapiganaji wake walikuwa wamejificha kwa miaka mingi katika Hifadhi ya wanyama ya Virunga, iliyoko katika wilaya ya Rutshuru ambapo waliishi kwa kufanya biashara ya miti na ujangili.

Sylvestre Mudacumura amekuwa anashtumiwa na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) uhalifu dhidi ya binadamu tangu mwaka 2013. Hata hivyo hakuweza kukamatwa.

Serikali ya DRC kwa muda mrefu imekuwa ikishtumiwa kumpa hifadhi na ulinzi. Lakini kwa mwaka mmoja, DRC ilitoa ahadi kwa serikali ya Kigali kuwa itawarudisha nyumbani wanamgambo wa FDLR, na miezi michache iliyopita msemaji wa kundi hilo alikabidhiwa serikali ya Kigali.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.