Familia ya Mugabe yakubali azikwe kwenye makaburi ya mashujaa jijini Harare
Familia ya rais wa zamani wa Zimbabwe Robert Mugabe imekubali kuwa rais huyo wa zamani azikwe kwenye makaburi ya mashujaa jijini Harare.
Imechapishwa:
Hatua hii inamaliza mvutano uliokuwa unashuhudiwa kati ya serikali na familia kuhusu ni wapi Mugabe aliyeongoza nchi hiyo kwa miaka 37 atazikwa.
Kutokana na uhusiano mbaya uliokuwepo kati ya Mugabe na rais Emmerson Mnangangwa aliyeingia madarakani, baada ya Mugabe kuondolewa madarakani na jeshi mwaka 2017.
“Wazee wa kijadi wameamua kuwa azikwe kwenye makaburi ya mashujaa, tunasubiri taarifa zaidi,” amesema Leo Mugabe msemaji wa Familia.
Hata hivyo, haijawa wazi iwapo atazikwa siku ya Jumapili kama ambavyo ilivyokuwa imepangwa hapo awali.
Familia yake ilikuwa inataka Mugabe aliyefariki dunia, akiwa na umri wa miaka 95 wiki iliyopita nchini Singapore azikwe katika kijiji cha Kutama alikozaliwa.
Mwili wa Mugabe, uliwasili jijini Harare siku ya Jumatano na wananchi wamekuwa wakitoa heshima zao za mwisho katika uwanja wa Rufaro.
Siku ya Jumamosi, kutakuwa na ibada ya kumkumbuka Mugabe katika uwanja wa taifa wa michezo jijini Harare na kuhudhuriwa na maelfu ya wananchi wa Zimbabwe wakiwemo viongozi mbambali wa Afrika akiwemo rais wa China Xi Jinping na rais wa zamani wa Brazil Raul Castro.