Mazungumzo kati ya pande mbili yasitishwa Sudan
Mamlaka nchini Sudan imetangaza kufungwa kwa shule zote kuanzia leo Jumatano hadi pale ambapo kutatolewa "amri ya kurudi shuleni".
Imechapishwa:
Tangazo hilo linakuja siku moja baada ya vifo vya waandamanaji sita wakiwemo wanafunzi wa shule tano za upili, waliouawa Jumatatu wakati wa maandamano katika mji wa Al-Obeid, katikati mwa nchi.
Vifo vya waandamanaji hao katika mji wa Al-Obeid, Kaskazini mwa Kordofan, pia vilisababisha kusitishwa kwa mazungumzo yaliyopangwa kufanyika Jumanne wiki hii kati ya viongozi wa waandamanaji na utawala wa kijeshi. Ujumbe wa waandamanaji katika mazungumzo hayo waliamua kuzuru mji huo.
Jumanne jioni, chama cha madaktari walio karibu na waandamanaji kilisema kwamba mwandamanaji wa sita alifariki dunia kutokana na majeraha aliyopata katika makabiliano na vikosi vya usalama, baada ya kupigwa "risasi kichwani", bila hata hivyo kuelezea kama alikuwa mwanafunzi wa shule ya upili.
Wanafunzi watano wa shule ya upili waliuawa na zaidi ya 60 walijeruhiwa, wengine walipigwa risasi kwa kuviziwa, wakati wa maandamano katika mji wa Al-Obeid, wakiandamana dhidi ya uhaba wa mkate na mafuta, kundi la waandamanaji na wakaazi wamesema.
"Kuua mwanafunzi ni kuua taifa", vijana walioandamana katika vitongoji kadhaa vya mji mkuu Khartoum wamekuwa wakiimba. Baadhi ya vijana hao walikuwa walivalia sare zao za shule, amesema mwandishi wa habari wa AFP.
Baraza la Kijeshi la Mpito "limewaamuru magavana wa majimbo yote kufunge shule za chekechea, shule za msingi na shule za upili kuanzia leo (Jumatano) hadi kutakapotolewa amri nyingine," kwa mujibu wa shirika la habari la serikali la SUNA.
Tangazo hilo linakuja wakati mamia ya wanafunzi wa shule ya upili na Vyuo Vikuu walikusanyika katika mji mkuu Khartoum Jumanne wiki hii kulaani vifo vya wenzi wao, wenye umri wa miaka 15 hadi 17 kwa mujibu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, (UNICEF).
Waandamanaji hao wanashtumu Kikosi cha cha wanamgambo (RSF), kinachoongozwa na kiongozi wa pili wa Baraza la Kijeshi linalotawala nchi hiyo, Mohammed Hamdan Daglo, kwa kufyatua risasi dhidi ya umati wa watu.
"Kuua raia wanaoandaman kwa amani ni jinai isiyokubalika ambayo haifai kubakia hivyo bila kuadhibiwa," mkuu wa Baraza la Kijshi la Mpito, Jenerali Abdel Fattah al-Burhane, amesema.
Siku ya Jumanne UNICEF ilitoa wito kwa mamlaka "kufanya uchunguzi na kuwafikisha wahusika wa unyanyasaji dhidi ya watoto mbele ya vyombo vya sheria ".