Pata taarifa kuu
SUDAN

Wanajeshi zaidi wasambazwa Khartoum na miji mingine

Baraza la kijeshi nchini Sudan limetuma wanajeshi zaidi kwenye mitaa ya jiji la Khartoum pamoja na miji mingine baada ya mwishoni mwa juma wananchi kuanza mgomo wa nchi nzima.

Waandamanaji wa Sudan wakiwa wamechoma moto matairi kwenye barabara za Khartoum
Waandamanaji wa Sudan wakiwa wamechoma moto matairi kwenye barabara za Khartoum Reuters
Matangazo ya kibiashara

Wiki moja baada ya kushuhudia mamia ya raia wakipoteza maisha wakishinikiza kurejeshwa kwa utawala wa kiraia, watu wanne wameuawa siku ya Jumapili wakati wanajeshi walipokuwa wakijaribu kuondoa vizuizi vilivyoanza kuwekwa na raia.

Vifo hivi vinatokea ikiwa ni karibu miezi miwili tangu April 11 wananchi na wanajeshi wafanikiwe kumuondoa mamlakani Omar al Bashir, wakati huu mazungumzo kati ya viongozi wa waandamanaji na wanajeshi yakigonga mwamba.

Waandamanaji walikuwa wakijaribu kuweka vizuizi kwenye barabara za mjini Khartoum huku masoko na maduka yakisaliwa yamefungwa kwenye maeneo mengi ya nchi.

Kamati ya madaktari ambao wako karibu na waandamanaji, wamesema watu wawili waliuawa katika makabiliano mjini Khartoum, wakati wengine wawili waliuawa katika mji wa Omdurman.

kamati hiyo imewalaumu wanajeshi wanaotii amri za viongozi wa kijeshi kwa kukabiliana kwa nguvu kubwa na waandamanaji, ambapo mpaka sasa jumla ya watu 118 wameripotiwa kupoteza maisha tangu Juni 3 mwaka huu.

Wizara ya afya inasema watu 61 wamepoteza maisha nchi nzima tangu kutekelezwa kwa operesheni ya kuwaondoa barabarani iliyoanza Jumatatu ya wiki iliyopita, 49 kati yao ikisema waliuawa kwa kupigwa risasi za moto.

Katika mji wa Kaskazini wa Bahari, raia walikuwa wakichoma moto matairi na kuweka mawe makubwa barabarani kama sehemu ya kuitikia wito wa viongozi wa waandamanaji.

Vurugu hizi zinajiri wakati huu viongozi wa kijeshi wakiwakamata wanasiasa wawili ambao mwishoni mwa juma lililopita walikutana na waziri mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed ambaye alienda nchini humo kujaribu kutafuta suluhuya kisiasa.

Umoja wa Afrika juma lililopita ulitangaza kuisimamisha uanachama Sudan hadi pale utawala wa kiraia utakapowekwa.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.