Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed azuru Sudan kuhimiza mazungumzo
Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed amezuru nchini Sudan kusaidia kurudisha mazungumzo kati ya uongozi wa kijeshi na viongozi wa waandamanaji baada ya mauaji ya zaidi ya watu 100 yaliyotokea wiki hii, kufuatia operesheni ya maafisa wa usalama, kuvunja kambi ya waandamanaji.
Imechapishwa:
Mazungumzo haya yalivunjika baada ya kutokea kwa machafuko jijini Khartoum, na licha ya jeshi kuomba radhi kwa mauaji hayo na kusema liko tayari kwa mazungumzo, viongozi wa waandamanaji wamekataa.
Aidha, viongozi wa waandamanaji wamekataa agizo la uongozi wa kijeshi kuwa, uchaguzi ufanyika baada ya miezi tisa baada ya kufuta makubaliano ya kuwepo kwa serikali ya mpito kwa kipindi cha miaka mitatu.
Ziara hii imekuja baada ya Umoja wa Afrika kuisimamisha Sudan kuwa mwanachama wa umoja huo, na kulitaka uongozi wa kijeshi kukabidhi madaraka kwa raia, hatua ambayo imeungwa mkono na mataifa ya Magharibi ikiongozwa na Umoja wa Ulaya.
Mzozo wa siasa nchini Sudan ulianza mwezi Desemba mwaka 2018, baada ya wananchi kuanza kuandamana wakilalamikia kupanda kwa gharama ya maisha lakini pia kushinikiza kujiuzulu kwa rais wa muda mrefu Omar Al Bashir.
Mwezi Aprili, Bashir alishinikizwa kujiuzulu baada ya waandamanaji kuamua kupiga kambi katika makao makuu ya jeshi jijini Khartoum.