Watu zaidi 150 watoweka baada ya boti kuzama katika Ziwa Kivu
Watu zaidi ya 150 hawajulikani waliko baada ya boti waliokuwa wakiabiri kuzama katika Ziwa Kivu, katika mkoa wa Kivu Kusini, mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo. Ajali ambayo ilitokea Jumatatu Aprili 15, 2019.
Imechapishwa:
Kwa mujibu wa mashahidi wakinukuliwa na shirika la Habari la Reuters, boti hilo ambalo lilikuwa limetoka katika mkoa jirani wa Kivu kaskazini lilizama katika Ziwa Kivu karibu na eneo la Kalehe.
Kwa mujibu wa chanzo cha polisi katika eneo la Kalehe miili mitatu iliopolewa na watu 33 wameokolewa.
Hata hivyo abiria wengine 150 hawajulikani waliko kufuatia ajali hiyo. Mamlaka inayosimamia safari za majini katika ziwa Kivu inasema kuwa idadi ya watu walioabiri chombo hicho haijulikani na wanahofu kuwa idadi ya watu 150 waliotoweka inaweza kuongezeka.
Akiwa ziarani mashariki mwa nchi hiyo, rais wa DRC Antoine Felix Tshisekedi Tshilombo amesema anafuatilia kwa karibu hali hiyo ili kuwatambua na kuwachukulia hatua kali waliohusika.
'Nimehuzunishwa na kuzama kwa boti, ajali iliyotokea tarehe 15 mwezi Aprili katika Ziwa Kivu. Hadi kufikia sasa idadi ya watu ambao hawajulikani waliko ni 150'' , arais wa DRC Felix Tshisekedi ameandika kwenye akaunti yake ya Twitter.
Ajali kama hizo zikitokea mara kwa mara nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
kulingana na shirika la afya duniani WHO, mwaka wa 2015, watu zaidi ya 100 walitoweka baada ya maboti mawili kugongana katika Mto Congo nchini DRC.