Uchaguzi nchini DRC: Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Ulaya kukutana
Mawaziri wa Mambo ya Kigeni wa Ulaya wanakutana Jumanne hii Januari 22 huko Brussels, nchini Ubelgiji kuangazia matokeo ya uchaguzi nchini DRC. Mawaziri wa Umoja wa Afrika wanatarajia kuhudhuria katika kikao hiki cha Baraza la masuala ya kigeni cha Umoja wa Ulaya.
Imechapishwa:
Baada ya ushindi wa Felix Tshisekedi Tshilombo katika uchaguzi wa Desemba 30 mwaka jana kuthibitishwa mwishoni mwa wiki hii na Mahakama ya Katiba na hatua ya Umoja wa Afrika ya kufuta ziara ya viongozi wa umoja huo mjini Kinshasa , baada ya kutilia mashaka matokeo ya uchaguzi siku ya Alhamisi, raia wengi wa DRC wanasubiri kuona kitakachotokea katika mkutano huo wa Brussels baada ya Umoja wa Ulaya pia kutilia mashaka matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa Desemba 30.
Umoja wa Ulaya unataka kwanza kukutana kwa mazungumzo na viongozi wa nchi za Afrika kabla ya kutoa msimamo wao wa pamoja. Umoja wa Ulaya kwa ombi la Ufaransa na Ubelgiji uliunga mkono wito wa Umoja wa Afrika kuitaka mamlaka nchini DRC kusitisha kutangaza matokeo ya uchaguzi wa urais, baaada ya Tume ya Uchaguzi nchini DRC (CENI) kumtangaza Felix Shisekedi mshindi wa uchaguzi huo.
Mwishoni mwa juma lililopita Martin Fayulu, aliyeshindwa katika uchaguzi wa urais, ambaye anadai kuwa alishinda lakini aliibiwa kura, aliomba jumuiya ya kimataifa kutomtambua Felix Tshisekedi kama rais wa DRC.
Tayari baadhi ya viongozi wa nchi kadhaa za Afrika kama vile Afrika Kusini, Kenya, Tanzania na Burundi wamempongeza Felix Tshisekedi kwa ushindi huo.