Pata taarifa kuu
DRC-SIASA-FAYULU-TSHISEKEDI

Fayulu awasilisha kesi ya kupinga ushindi wa Tshisekedi

Mgombea urais kupitia muungano wa upinzani wa Lamuka nchini DRC Martin Fayulu, amewasilisha kesi katika Mahakama ya Katiba kupinga, ushindi wa Felix Tshisekedi, aliyetangazwa wiki hii na Tume ya Uchaguzi kuwa alishinda uchaguzi wa urais uliofanyika tarehe 30 mwezi Desemba mwaka 2018.

Martin Fayulu, mgombea wa upinzani nchini DRC
Martin Fayulu, mgombea wa upinzani nchini DRC REUTERS/Baz Ratner
Matangazo ya kibiashara

Wakili wa Fayulu, Feli Ekombe amewaambia wanahabari jijini Kinshasa kuwa, kesi hiyo iliwasilishwa siku ya Ijumaa, na mgombea huyo anataka matokeo yaliyompa ushindi Tshisekedi, yafutwe.

Tume ya Uchaguzi ilimtangaza Tshisekedi mshindi, kwa kupata asilimia 38.57 ya kura zote zilizopigwa huku Fayulu akiwa wa pili kwa asilimia 34.8.

Mgombea wa chama tawala Emmanuel Ramazani Shadary, aliambulia asilimia 23.8.

Hata hivyo, Fayulu tayari amesema alishinda uchaguzi huo kwa kupata asilimia 61 ya kura zote.

Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki, waliokuwa na waangalizi zaidi ya 40,000 kote nchini humo, limesema matokeo yaliyotangazwa hayakuwa sahihi.

Kauli hii ya Kanisa Katoliki, imeungwa mkono na mataifa ya magharibi kama Ufaransa, Uingereza, Ubelgiji huku Marekani ikisema inataka ukweli kufahamika.

Uamuzi unatarajiwa kufanywa na Mahakama ndani ya wiki moja.

Wakati uo huo, vyama vinavyomuunga mkono rais Joseph Kabila anayeondoka madarakani, kimepata idadi kubwa ya wabunge.

Shirika la Habari la Ufaransa AFP linasema, kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa na Tume ya Uchaguzi, muungano wa chama tawala umepata zaidi ya viti 250 katika bunge hilo la wabunge 500 na kupita nusu, inayotakiwa ili kuongoza bunge hilo.

Hadi sasa vyama vinavyomuunga rais Kabila vimepata viti 288, huku upinzani ukipata viti 141 kati ya maeneo bunge ambayo zoezi la kuhesabu kura limemalizika.

Zaidi ya wagombea 15,000 walijitokeza kuwania nafasi ya kwenda bungeni.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.