Pata taarifa kuu
DRC-SIASA-USALAMA

Kura zaendelea kuhesabiwa DRC

Zoezi la kuhesabu kura linaendelea nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, baada ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika Jumapili Desemba 30 kuahirishwa mara kadhaa nchini humo.

Zoezi la kuhesabu kura katika moja ya vituo vya kupigia kura mjini Goma, Desemba 30, 2018
Zoezi la kuhesabu kura katika moja ya vituo vya kupigia kura mjini Goma, Desemba 30, 2018 © PATRICK MEINHARDT / AFP
Matangazo ya kibiashara

Wakati huo huo wagombea wakuu wa upinzani Felix Tshisekedi na Martin Fayulu wamelalamikia dosari nyingi wanazodai kwamba zilitokea wakati wa uchaguzi huo.

Felix Tshisekedi, mtoto wa kiongozi wa upinzani wa kihistoria nchini DRC, Etienne Tshisekedi, amesema anahofia kwamba huenda hitilafu hizo zilipangwa ndipo kutoa sababu za uchaguzi kufutwa katika baadhi ya maeneo na kumuwezesha Bw Kabila kusalia madarakani.

Zoezi la kupiga kura lilimalizika usiku katika maeneo mengi ya DRC huku changamoto kadhaa zikiripotiwa katika maeneo mbalimbali.

Ripoti kutoka kwa mwandishi wetu Sonia Rolley zinasema baadhi ya vituo vya kupigia kura katika eneo la Inongo vilichomwa moto.

Zaidi ya wapiga kura milioni 40 walijiandikisha katika daftari la kupigia kura lakini idadi ya waliojitokeza huenda ikawa pungufu. Hata hivyo bado ripoti kutoka maeneo mbalimbali ya taifa hilo hazijabainisha kwa kina namna zoezi la upigaji kura lilivyoendeshwa.

Mapema jana Jumapili mvua ilitatiza shughuli za upigaji kura katika Jiji la Kinshasa.

Baadhi ya wanaharakati waliandaa uchaguzi wa mwisho uliopewa jina 'uchaguzi wa raia' katika miji ya Beni na Butembo, katika mkoa wa Kivu Kaskazini, mashariki mwa DRC, lakini Tume Huru ya Uchaguzi imesema kura hiyo sio halali.

Uchaguzi uliahirishwa katika maeneo yaliyoathiriwa na Ebola yakiwemo miji ya Beni na Butembo mashariki mwa nchi hiyo, na pia katika jiji la Yumbi magharibi mwa nchi hiyo kutokana na mdororo wa usalama. Miji hiyo inadaiwa kuwa ni ngome ya upinzani.

Tume ya uchaguzi inatazamiwa kuanza zoezi la kuhesabu kura lakini mshindi wa kiti cha urais atatangazwa Januari 15 na kuapishwa Januari 18.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.