Wafuasi wa mgombea wa upinzani Fayulu wasambaratishwa Lubumbashi
Polisi nchini DRC imewatawanya wafuasi wa mgombea wa upinzani Martin Fayulu karibu na uwanja wa ndege wa Lubumbashi ambako walikuwa wanamsubiri kiongozi wao katika kampeni ya uchaguzi wa urais uliopangwa kufanyika Desemba 23.
Imechapishwa:
Mamia ya wafuasi wa mgombea huyo waliokuwa wakiongozana kumlaki kiongozi wao wametawanywa kwa mabomu ya machozi na kurushiwa maji ya moto karibu na sehemu ya kuegesha magari kwenye uwanja wa ndege, kwa mujibu wa mwandishi wa habari wa AFP.
Magari kumi ya polisi na malori kadhaa ya kikosi cha kutuliza ghasia yamekuwa yameegesha karibu na uwanja wa ndege wa Lubumbashi, mji wa pili wa DRC na mji mkuu wa nchi hiyo kwa madini ambao unapiganiwa na utawala na upinzani.
Hata hivyo Martin Fayulu amewasili katika uwanja wa ndege wa Lubumbashi na kuondoka akiwa ndani ya gari ndogo, huku msafara wake ukiwa chini ya ulinzi mkali wa polisi hadi katikati ya mji ambako anatarajia kuendesha kampeni yake.
Mmoja wa wanasiasa wakuu wanaomuunga mkono ni gavana wa zamani wa Katanga na mtu maarufu Lubumbashi, Moise Katumbi, aliye uhamishoni nchini Ubelgiji.
Lubumbashi pia ni ngome ya rais wa sasa, Joseph Kabila, ambapo "mgombea wake", Emmanuel Ramazani Shadary, alianza kampeni yake Novemba 26.
Upinzani umegawanyika kati ya Bw Fayulu na Felix Tshisekedi, mgombea wa chama cha kihistoria cha UDPS, ambaye alitoa saini yake kwenye mkataba wa Geneva kuhusu uteuzi wa mgombea mmoja, saa 24 baada ya kutia saini.