Libya: Kura ya maoni kuhusu katiba kupigwa mwishoni mwa Februari
Kura ya maoni kuhusu katiba mpya nchini Libya inaweza kupigwa mnamo mwezi Februari 2019, ikiwa hali ya usalama itaimarika, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (HNEC) ametangaza.
Imechapishwa:
"Inawezekana kuandaa kura ya maoni kuhusu rasimu ya Katiba (...) mwishoni mwa mwezi Februari" 2019, amesema Imed al-Sayeh, mwenyekiti wa Tume Taifa ya Uchaguzi (HNEC) katika mkutano na waandishi wa habari.
Masharti ya kwanza "yametimizwa na kupitishwa kwa sheria "kuhusu kura ya maoni". Sheria ambayo imepitishwa nabunge lililochaguliwa na lenye makao yake makuu mashariki mwa nchi, "hata kama halitimizi idadi," Sayeh amesema.
Hata hivyo, amesema kwamba akaunti ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi iko kama tupu wakati inahitaji dinari milioni 40 (karibu dola milioni 30) kutekeleza operesheni ya uchaguzi.
Zoezi hilo la kura ya maoni pia litategemea na hali ya usalama, "changamoto kubwa," kwa mujibu wa Sayeh.
Libya inaendelea kukabiliwa na machafuko na mashambulizi ya hapa na pale tangu kuanguka kwa utawala wa Muammar Gaddafi mwaka 2011.
Mnamo mwezi Mei HNEC ilikumbwa na shambulio baya, lililodaiwa kutekelezwa na kundi la Islamic State (IS). Watu kumi na wanne waliuawa katika shambulizi hilo, ikiwa ni pamoja na wafanyakazi watatu wa tume hiyo.