Pata taarifa kuu
DRC-UN-USALAMA

Umoja wa Mataifa watafuta walinda amani wawili waliotoweka DRC

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini DRCongo umeanza kuwatafuta askari wake wawili waliotoweka tangu kuzuka kwa maigano mwezi Novemba katika eneo la Beni, mashariki mwa nchi hiyo.

Jeshi la Monusco likishirikiana na jeshi la DRC, FARDC, wakati wa operesheni ya pamoja katika eneo la Beni, Oktoba 2017.
Jeshi la Monusco likishirikiana na jeshi la DRC, FARDC, wakati wa operesheni ya pamoja katika eneo la Beni, Oktoba 2017. MONUSCO
Matangazo ya kibiashara

"Kipaumbele cha ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini DRC (MONUSCO) ni kuwapata askari wawili waliotoweka mwezi Novemba na kuna vipeperushi ambavyo vimewekwa katika maeneo mbalimbali ya msitu ili kuwasaidia kujiunga na wenzao," amesema Florence Marchal, msemaji wa MONUSCO, katika mkutano na waandishi wa habari mjini Kinshasa.

Askari hao walikuwa wakishiriki mwezi uliopita katika operesheni ya pamoja ya kijeshi ya vikosi vya Umoja wa Mataifa nchini DRC (MONUSCO) na jeshi la DRC dhidi ya waasi wa Uganda wa Allied Democratic Forces (ADF) katika eneo la Beni katika mkoa wa Kivu Kaskazini.

"Kwa upande wa MONUSCO, askari wanne walitoweka lakini, wawili walipatikana wakiwa salama," amesema Bi Marchal.

"Idadi ya watu waliouawa katika mapigano hayo sasa imefikia 7 na wengine 13 ambao walijeruhiwa, ikiwa ni pamoja na Walinda amani wawili , ameongeza, akimaanisha mapigano yaliyotokea Novemba 14.

Operesheni ya kijeshi ya pamoja dhidi ya ADF inaendelea katika eneo la Beni, eneo ambalo kwa wiki chache zilizopita halikushuhudia mashambulizi kutoka kundi hilo au makundi mengi ya watu wenye silaha, kwa mujibu wa msemaji wa MONUSCO.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.