Rais Bouteflika kuwania katika uchaguzi wa urais wa mwaka 2019 Algeria
Rais wa Algeria Abdelaziz Bouteflika, mwenye umri wa miaka 81, atapeperusha bendera ya chama cha National Liberation Front (FLN), katika uchaguzi wa urais uliopangwa kufanyika mwezi Aprili 2019, Djamel Ould Abbes, kiongozi wa chama cha FLN amesema, akinukuliwa na shirika la Habari la serikali APS.
Imechapishwa:
Akishinikizwa na kambi yake kuwania kwa muhula wa tano tangu miezi sita iliyopita, Rais Bouteflika, ambaye hali yake ya afya imekuwa ikidhoofika kufuatia maradhi ya kiharusi (CVA) yanayomkabili tangu mwaka 2013, bado hajaelezea kuhusua suala hilo.
"Rais Bouteflika, pia rais wa chama, ni mgombea wa chama cha FLN kwa uchaguzi wa urais wa mwaka 2019," amesema Bw Ould Abbes katika sherehe kwa heshima ya Mkuu mpya wa kundi la wabunge wa chama tawala Mohamed bouabdallah.
"Bouteflika kuwania katika uchaguzi wa mwaka 2019 ni ombi la makada wote wa chama cha FLN na wafuasi wa chama hicho nchini kote," Bw Ould Abbes ameongeza, kwa mujibu wa shirika la Habari la serikali la APS.
Kamati Kuu ya chama cha FLN itakutana hivi karibuni ili kurasimisha uteuzi, mkurugenzi wa ofisi ya Ould Abbes, Nadir Boulegroune, ameliambia shirika la Habrai la AFP.
Mnamo mwezi Aprili 2014, alichaguliwa tena kwa muhula wa nne, karibu mwaka mmoja baada ya kupata kiharusi, alilazwa kwa muda wa miezi mitatukatika hospitali ya Paris.
Bouteflika, ambaye alipata kiharusi 2013 na afya yake kudhoofika, na kulazimika kutumia kiti cha magurudumu, amekuwa akiongoza Algeria tangu mwaka 1999.