Chama kikuu cha upinzani nchini Msumbiji Renamo, chakataa kushiriki katika mazungumzo ya amani
Chama kikuu cha upinzani nchini Msumbiji cha Democratic Renewal of Mozambique ambacho pia kinafahamika kama Renamo, kimetangaza kuahirisha ushiriki wake katika mazungumzo ya amani na Serikali kikipinga matokeo ya uchaguzi wa serikali za mitaa.
Imechapishwa:
Msemaji wa Renamo, Andre Magibire amewaambia waandishi wa habari mjini Maputo kuwa, chama chao sasa kinajikita katika kutatua changamoto za uchaguzi zilizoshuhudiwa baada ya uchaguzi wa October 10.
Kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa na Tume ya Uchaguzi, yameonesha kuwa chama tawala cha Frelimo kimepata viti 44 huku Renamo kikipata viti 8, matokeo ambayo sasa kimeyakataa kikisema kulikuwa na udanganyifu mkubwa.
Wakuu wa chama hicho wanasema kuwa suluhu ya changamoto za uchaguzi zilizoshuhudiwa ndio kitu pekee kitakachowafanya warejee tena katika meza ya majadiliano ya amani na Serikali.
Hivi karibuni pande hizo mbili zilikubaliana kuwepo kwa ugavi wa madaraka katika ngazi ya kaunti pamoja na kuingizwa jeshini kwa wapiganaji wa Renamo.