Polisi Tanzania yaapa kuwashughulikia waliomteka Mo Dewji
Baada ya kuachiliwa huru mfanyabiashara bilionea Mohamed Dewji aliyetekwa kwa takribani siku 9 jijini Dar es salaam jeshi la polisi nchini Tanzania limeahidi kuwasaka na kuwatia nguvuni wahusika wa utekaji huo.
Imechapishwa:
Mkuu wa jeshi la polisi nchini Tanzania, Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) Simon Sirro ameahidi kuwapata wakiwa wazima au wamekufa.
Aidha Kamishna msaidizi muandamizi wa jeshi la Polisi ambae pia ni kamanda wa kanda maalum ya polisi Dar es salaam Lazaro Mambo Sasa amesema kulingana na taarifa za hapo awali kwamba waliomteka Mo sio raia wa Tanzania, zimethibitishwa na Mo mwenyewe ambae amesema wahalifu walikuwa wanatumia lugha inayofanana na lugha inayotumiwa huko nchini Afrika Kusini.
Mohamed Dewji ameonekana mwenye uchovu aliongea kwa unyonge na kutoa shukrani za dhati kwa mwenyezi Mungu kwa rais John P Magufuli na Watanzania wote.
Mohamed Dewji alitekwa Alhamisi iliyopita na watu wasiojulikana na kuachiwa jumamosi kwa kutelekezwa katika viwanja vya Jimkana jijini Dar es Salaam.