Mtu mmoja auawa na 17 watekwa nyara karibu na Beni
Mtu mmoja ameuawa na wengine 17 wametekwa nyara katika shambulizi jipya la kundi la waasi wa Uganda la Allied Democratic Forces (ADF). Shambulizi ambalo lilitokea Jumatatu jioni katika mji wa Oicha mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, vyanzo vya kiraia na utawala vimesema leo Jumanne.
Imechapishwa:
Nyumba nne zilichomwa moto na mbuzi na kuku waliibwa wakati wa shambulizi hilo siku mbili baada ya mauaji ya watu zaidi ya ishirini katika mji jirani wa Beni, shambulizi ambalo lilihusishwa kundi la "kigaidi" la ADF.
"Hali imezorota katika mji wa Oicha," afisa wa serikali, Donat Kibwana amesema Jumanne wiki hii. Maduka mengi na shule vimefungwa.
Shambulizi hili jipya la Jumamosi na leo Jumatatu limezua hofu na hasira miongoni mwa wakaazi wa eneo la Beni (Kivu Kaskazini) ambako mamia ya raia wameuawa tangu Oktoba 2014 katika mauaji yaliyohusishwa kundi la ADF.
Muungano wa mashirika ya kiraia mjini Beni mkoani Kivu Kaskazini yametowa wito kwa wananchi wa eneo hilo kuongeza siku za mambolezo hadi Ijumaa wiki hii.
Mashirika hayo pia yameomba viongozi wa kiraia na wa kijeshi katika eneo hilo kujiuzulu baada ya kushindwa kuzuia shambulizi dhidi ya raia mwishoni mwa juma lililopita ambalo lilitekelezwa na waasi wa ADF.