Hatima ya kisiasa ya Jean-Pierre Bemba kujulikana Jumatatu hii
Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ICC inatarajia kutoa uamuzi wake dhidi ya kiongozi wa zamani wa kivita ncini DRC, Jean-Pierre Bemba baada ya kupatikana na hatia ya kuhonga mashahidi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Wakati huo huo Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imetishia kujitoa kwenye mahakama hiyo iwapo itabadilisha uamuzi dhidi ya kiongozi huyo wa zamani wa kivita ambaye pia ni kiongozi wa chama kikuu cha upinzani cha MLC.
Wizara ya mambo ya nje ya DRC imeshtumu kwamba Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ICC imekua sasa ni chombo kinachonufaisha baadhi ya mataifa huku kuyakandamiza mataifa mengine.
Taarifa hiyo imesema kuwa ICC imekuwa ikipata shinikizo kutoka kwa baadhi ya nchi na hali hiyo inaweza kuhatarisha chombo hicho kinapoteza uamunifu wake.
Mahakama ya Katiba ilithibitisha uamuzi wa CENI wa kumzuia Jean- Pierre Bemba kuwania katika uchaguzi wa urais wa Desemba 23 na kusema kuwa hana sifa ya kuwania katika uchaguzi huo kufuatia hukumu aliyopewa na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) kwa kosa la kuhonga mashahidi.
Hivi karibuni chama cha kiongozi wa zamani wa kivita Jean-Pierre Bemba kilitoa wito kwa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu "kuweka mambo sawa" kuhusu sheria iliyomhukumu Bemba kwa kosa la kuhonga mashahidi.
Jean-Pierre Bemba anatajwa kama mpinzani mkuu anayesumbua utawala wa Joseph Kabila na chama chake cha PPRD katika uchaguzi ujao.
Hivi karibuni Bemba aliachiliwa katika kesi dhidi ya uhalifu wa kivita na mahakama baada ya kutumikia kifungo cha miaka kumi jela.
Mwezi uliopita alirejea nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na kupokelewa kwa mapokezi makubwa kutoka kwa wafuasi wake.