Roketi zaanguka kando ya uwanja wa ndege wa Tripoli
Mapigano yanaendelea nchini Libya, hasa karibu na mji mkuu wa nchi hiyo Tripoli. Kwa mujibu wa chanzo cha mamlaka ya uwanja wa ndege wa Tripoli, roketi kadhaa zimeanguka pembezoni mwa uwanja huo, bila hata hivyo kusababisha hasara yoyote.
Imechapishwa:
Ndege ya shirika la ndege la Libya la Libya Airlines ambayo imekua ikifanya safari kati ya Alexandria (Misri) na Tripoli imeamua kutua katika uwanja wa ndege wa Misrata, kilomita 200 mashariki kutoka mji mkuu wa Libya, chanzo hicho ambacho hakikutaja jina kimesema.
"Maandalizi yanaendelea kuhusu kuhamisha ndege kutoka Mitiga" kwenda Misrata, chanzo hicho kimesema.
Uwanja wa ndege wa Mitiga, kaskazini mwa Tripoli, ulifungwa kuanzia Agosti 31 hadi Septemba 6 kutokana na mapigano kati ya makundi hasimu ya waasi karibu na mji mkuu.
Angalau makombora matatu yalianguka karibu na uwanja wa ndege mwishoni mwa Agosti, na kupelekea mamlaka ya uwanja wa ndege kufuta safari za ndege na hivyo kuzitaka ndege kuthamia kwenye uwanja wa ndege wa Misrata.
Uwanja wa ndege wa Mitiga ulifunguliwa upya Septemba 7 baada ya kutiliwa saini, chini ya mwamvuli wa Umoja wa Mataifa, mkataba wa kusitisha mapigano kati ya wanamgambo hasimu waliohusika katika makabiliano makali kusini mwa Tripoli.