Bemba kurejea Ulaya baada ya kuwasilisha ombi la kuwania urais
Mwanasiasa wa upinzani nchini DRC Jean-Pierre Bemba anatarajiwa kurejea barani Ulaya siku ya Jumapili, baada ya kufanikiwa kuwasilisha ombi lake la kuwania urais kwa Tume ya Uchaguzi wiki hii.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Bemba ambaye amewahi kuwa Makamu wa rais aliwasili nyumbani siku ya Jumatano wiki hii na kulakiwa na maelfu ya wafuasi wake, kabla ya kufanikiwa kufika katika Ofisi za Tume ya Uchaguzi.
Mwanasiasa mwingine wa upinzani Moise Katumbi Chapwe alizuiwa kuingia nchini humo siki ya Ijumaa, akiwa mpakani kati ya nchi yake na Zambia, hatua ambayo Bemba amelaani.
Katumbi amesema, atahakikisha kuwa anarejea nyumbani kabla ya kumaliza kwa zoezi la kuwasilisha ombi la kuwania urais wiki ijayo.
"Nimezuiwa kuingia nchini mwangu, kosa langu ni nini, nimekuja kuwasilisha maombi ya kuwania urais, nitapambana," aliandika Katumbi kwenye ukurasa wake wa Twitter.
Rais Joseph Kabila, ambaye kikatiba haruhusiwi kuwania urais, inasubiriwa kuona iwapo wiki ijayo atawasilisha ombi la kutaka kuwania tena kwa muhula mwingine.
Uchaguzi Mkuu umepangwa kufanyika tarehe 23 mwezi Desemba.