Human Right Watch yaionyooshea kidole cha lawama Cameroon
Shirika la kutetea haki za Binadmau la Human Rights Watch limeishtumu serikali ya Cameroon kwa machafuko yanayoendelea katika maeneo ambayo raia wa nchi hiyo wanazungumza lugha ya Kiingereza.
Imechapishwa:
Human Rights Watch inasema serikali imeshindwa kuzuia kuuawa kwa raia wa kawaida wa nchi hiyo lakini pia kusababisha zaidi ya watu 180,000 kuyakimbia makwao.
Wanaharakati hao sasa wanataka Jumuiya ya Kimataifa, kuwasaidia wakaazi wa Magharibi na Kusini mwa nchi hiyo ambao haki zao zinakiukwa.
Hata hivyo wadadisi wanasema machafuko hayo yamesababishwa kwa upande mmjoa na wanaharakati wanaotaka kujitenga kwa eneo lao na kuwa taifa huru, na kwa upande mwengine vikosi vya usalama.
Hivi karibuni serikali ilishtumu wanaharakati hao kuhusika katika mauaji ya askari wake zaidi ya 80, madai ambayo wanaharakati hao walitupilia mbali.
Viongozi kadhaa wa wanaharakati hao waliokamatwa nchini Nigeria na kukabidhiwa serikali ya Cameroon wanaendelea kuzuiliwa katika jela mbalimbali nchini humo.
Serikali ya Cameroon inasema imewaruhusu maafisa wa shirika la msalaba mwekundu kukutana na kiongozi mkuu wa kundi hilo, ambaye ni miongoni mwa wanaharakati zaidi ya arobaini wanaozuiliwa na utawala wa Paul Biya.