Pata taarifa kuu
ZIMBABWE

Zimbabwe: 41 walijeruhiwa, rais asema wakati wake wa kufa haujafika

Waziri wa afya nchini Zimbabwe amesema jumla ya watu 41 walijeruhiwa katika mlipuko ambao ulitokea saa chach baada ya rais wa nchi hiyo Emmerson Mnangagwa kumaliza kuhutubia mkutano wa kampeni za kuelekea uchaguzi mkuu wa mwezi Julai.

Rais wa Zimbabwe, Emmerson Mnangagwa wakati akihutubia mkutano wa hadhara mjini Bulawayo, 23.06.2018
Rais wa Zimbabwe, Emmerson Mnangagwa wakati akihutubia mkutano wa hadhara mjini Bulawayo, 23.06.2018 Tafadzwa Ufumeli/via REUTERS
Matangazo ya kibiashara

Waziri David Parirenyatwa amesema miongoni mwa waliojeruhiwa kwenye mlipuko huo ni pamoja na mke wa makamu wa rais, spika wa bunge na manaibu wake wawili.

Waziri Parirenyatwa ameongeza kuwa majeruhi wanatibiwa kwenye hospitali kubwa tatu za mji wa Bulawayo na wengi wanalalamika kuhusu maumivu.

Picha za video zinaonesha mlipuko huo kutokea saa mita chache tu tangu rais Mnangagwa na wapambe wake washuke kwenye ngazi za jukwaa, katika tukio ambalo ni wazi lilikuwa ni la jaribio la kumuua.

Rais Mnangagwa mwenyewe amesema shambulio hilo lililenga kumuua ambapo liliwajeruhi makamu wake wawili wa rais Kembo Mohadi na Constantino Chiwenga.

Watoa huduma ya kwanza wakiwasaidia majeruhi wa mlipuko kwenye uwanja wa Bulawayo wakati rais Mnangagwa akihutubia, 23.06.2018
Watoa huduma ya kwanza wakiwasaidia majeruhi wa mlipuko kwenye uwanja wa Bulawayo wakati rais Mnangagwa akihutubia, 23.06.2018 Tafadzwa Ufumeli/via REUTERS

“Kifaa kililipuka sentimita chache na nilipokuwa, lakini bado sio muda wangi”, amesema rais Mnangagwa wakati alipohojiwa na kituo cha televisheni ya taifa hapo jana.

“Hawa ni maadui zangu waliokufa na majaribio haya yamekuwa mengi maishani mwangu”.

“Sio Jaribio la kwanza la maisha yangu. Nimeshazoea. Zaidi ya mara sita ofisi yangu ilivamiwa, vifaa vya mlipuko viliwekwa mara nyingi tu. Nitaendelea bado.”

Waziri wa afya ameongeza kuwa wengi waliojruhiwa wamepoteza baadhi ya viungo vyao kama mkono na mguu na wengine wanahitaji operesheni za haraka na dharula na kwamba Serikali itaendelea kurekodi idadi ya watu waliojeruhuwa.

Mnangagwa ambaye aliondolewa haraka kwenye eneo la tukio, baadae alionekana kuwatembelea majeruhi waliokuwa hospitali.

Licha ya kuwa mji wa Bulawayo unafahamika kama ngome kubwa ya upinzani dhidi ya chama tawala cha ZANU-PF na ulikuwa ni mkutano wa kwanza kwa rais Mnangagwa kwenye mji wa Bulawayo, wadadisi wa mambo wanasema viashiria vyote vinaonesha kuwa ni watu wake wa ndani hasa kutokana na mzozo unaoendelea kufukuta ndani ya chama tawala.

Nchi ya Zimbabwe itafanya uchaguzi wake mkuu wa urais katika kipindi cha wiki tano zijazo tangu kung’olewa madarakani kwa aliyekuwa rais wa nchi hiyo kwa zaidi ya miaka 37 Robert Mugabe.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.