Jamhuri ya Afrika ya Kati yachukua tahadhari dhidi ya Ebola DRC
Kutokana na kuongezeka kwa maambukizi ya Ugonjwa hatari wa Ebola nchini DRC, nchi jirani kama Jamhuri ya Afrika ya kati pamoja na Congo Brazzaville zimechukua tahadhari kwenye maeneo ya mpakani.
Imechapishwa:
Wizara ya afya Mjini Bangui imesitisha safari za ndege kutoka Mji wa Mbandaka kuelekea Bangui, kwa muda usiojulikana.
Hayo yanajiri wakati ambapo Kanisa Katoliki nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, linasema lina wasiwasi kuhusu kuendelea kuripotiwa kwa maambukizi mapya ya virusi hatari vya Ebola Kaskazini Magharibi mwa nchi hiyo.
Hadi sasa watu 25 wamepoteza maisha na 54 kuambukizwa, huku wengine 1,139 wakiwa wanachunguzwa kwa karibu baada ya kuwa karibu na watu waliambukizwa.
Kauli hii imetolewa na Askofu wa Kanisa hilo Fridolin Ambongo ambaye ametembelea mji wa Mbandaka na Bikoro maeneo ambayo yameathiriwa na ugonjwa huo.
Askofu Ambongo amesema, hofu imetenda kote katika maeneo yaliyoathiriwa na Kanisa Katoliki, limesitisha kwa muda mikutano ya hadhara ikiwepo, ubatizo na ibada ya kuwasimika makasisi iiyokuwa imepangwa kufanyika tarehe 3 mwezi ujao katika mji wa Mbandaka, imeahirishwa.
Kanisa hilo, limeugana na maafisa wa afya kutoa wito kwa wakaazi wa Kaskazini Magharibi mwa nchi hiyo, kuacha kusaliamiana au hata kugusana na kunawa mikono yao kwa sabuni na maji safi, ili kuepuka kuambukizwa ugonjwa huo.
Shirika la afya duniani WHO, nalo limeedelea kutoa chanjo katika njia mojawapo ya kupambana na ugonjwa huu hatari.