Pata taarifa kuu
DRC-UTALII-USALAMA

Watalii wawili kutoka Uingereza waliotekwa waachiliwa DRC

Watalii wawili, raia wa Uingereza waliotekwa nyara siku ya Ijumaa wiki iliyopita katika Hifadhi ya Wanyama ya Virunga katika moka wa Kivu Kaskazini, mashariki mwa DRC, wameachiliwa.

Hifadhi ya Taifa ya Wanyama ya Virunga karibu na Rutshuru tarehe 17 Juni 2014 (picha ya kumbukumbu).
Hifadhi ya Taifa ya Wanyama ya Virunga karibu na Rutshuru tarehe 17 Juni 2014 (picha ya kumbukumbu). Junior D. Kannah / AFP
Matangazo ya kibiashara

Watalii hao waliachiliwa siku ya Jumapili, Mei 13 pamoja na dereva wao, raia wa DRC. Taarifa hii imethibitishwa na wizara ya mambo ya nje ya Uingereza na uongozi wa Hifadhi ya Wanyama ya Virunga.

Kwa mujibu wa vyanzo kutoka eneo hilo, gari la mamlaka ya Hifadhi ya Wanyama (ICCN) lilikua likielekea Goma pamoja na watalii wawili kutoka Uingereza, wakisindikizwa na walinzi wa Hifadhi hiyo, walishambuliwa na watu wenye silaha kati ya Kilimanyoka na Kibumba, eneo la Nyiragongo.

Wakati wa shambulio hili, mlinzi mmoja wa Hifadhi ya Wanyama ya Virunga aliuawa. Rachel Baraka, mmoja wa wanawake 26 jasiri wanaohudumu katika Hifadhi ya Wanyama ya Virunga, alifariki dunia kutokana na majeraha alioyapata. Mamlaka ya Hifadhi ya Wanyama ya Virunga imemsifu. Hakuna maelezo yaliyotolewa kuhusu utambuzi wa washambuliaji au ikiwa kuna malipo yoyote ya fidia yaliyotolewa.

Tukio hilo lilitokea katika eneo ambalo jeshi la Jamhuri ya Congo (FARDC) limekua likikabiliana na makundi mbalimbali ya watu wenye silaha katika hifadhi hiyo. Saa chache baada ya kisa hicho cha utekaji nyara, jeshi la DRC liliendesha doria katika hifadhi hiyo kwa minajili ya kuwapata hai mateka hao.

Ikumbukwe kuwa mnamo Mei 1, watu wasiopungua wanne waliuawa katika mashambulizi ya watu wenye silaha waliodai kuwa ni waasi wa FDLR, kundi la wasi wa Kihutu wa Rwanda, dhidi ya msafara wa magari ya wafanyabiashara katika Hifadhi ya Wanyama ya Virunga.

Kulingana na taarifa zilizokusanywa na RFI, katika siku zilizotangulia shambulio, Mamlaka ya Hifadhi ya Wanyama (ICCN) ilitishiwa kwa kuweka kizuizi katika eneo la Kibumba katika kupambana dhidi ya biashara ya makaa, ambayo kwa mujibu Umoja wa Mataifa umetajirisha baadhi ya makundi ya watu wenye silaha, kama maafisa wa jeshi la DRC huko mashariki mwa nchi. Haikuwa mbali na Kibumba ambapo kulitokea shambulizi dhidi ya gari mamlaka ya Hifadhi ya Wanyama (ICCN) siku ya Ijumaa.

Onyo hili lilitolewa na FDLR, waasi wa Kihutu wa Rwanda, au washirika wao kutoka DRC, Nyatura, ambao wanashutumiwa kutekeleza shambulio hili.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.