Wanajeshi 12 wauwa baada ya uvamizi wa Ubalozi wa Ufaransa na Makao makuu ya jeshi jijini Ouagadougou
Wanajeshi wanane na wengine 12 walijeruhiwa baada ya watu waliokuwa wamejihami kwa silaha kuvamia ubalozi wa Ufaransa na Makao Makuu ya Jeshi jijini Ouagadougou nchini Burkina Faso, siku ya Ijumaa.
Imechapishwa:
Ripoti za kiusalama kutoka kwa serikali ya Ufaransa zimethibitisha mauaji haya na kuongeza kuwa wavamizi wengine wanane waliuawa katika makabiliano hayo makali.
Awali, kulikuwa na ripoti kuwa mashambulizi hayo ambayo pia yalilenga makao makuu ya jeshi la Burkina Faso yalisabisha vifo vya watu 28.
Serikali ya Burkina Faso imesema inachunguza tukio hilo, ili kuwatambua waliotekeleza mashambulizi hayo mabaya hivi karibuni nchini humo.
Hakuna kundi lililojitokeza kudai kuhusika lakini makundi ya kijihadi yameendelea kuwa tishio kwa serikali ya Burkina Faso na mataifa ya ukanda wa Sahel kama Niger, Chad, Mali na Mauritania.
Waziri wa usalama wa Burkina Faso Clement Sawadogo amesema watu wawili walikamatwa nje ya makao makuu ya jeshi wakati wa uvamizi huo, na kuongeza kuwa uchunguzi wa awali umeonesha kuwa kulikuwa na gari lililokuwa limejazwa vilipuzi.
Ufaransa ambayo imetuma wanajeshi wake 4,000 katika ukanda wa Sahel, imesema ililengwa katika uvamizi huo.