Mkutano kuhusu misaada kwa wakimbizi wa DRC kufanyika Aprili 13
Wafadhili mbalimbali wanatarajiwa kukutana mwezi ujao kuchangisha Dola Bilioni 1.7 kufanikisha misaada ya kibinadamu kuwasaidia mamilioni ya wakimbizi nchini DRC.
Imechapishwa:
Hatua hii imetangazwa na Umoja wa Mataifa, ambao umesema unahitaji fedha hizo kufanikisha miradi yake katika taifa hilo ambalo limekumbwa na ukosefu wa usalama eneo la mashariki na katika jimbo la Kasai.
Mkutano huo umepangwa kufanyika tarehe 13 mwezi ujao jijini Geneva nchini Uswisi.
Wiki mbili zilizopita Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Wakimbizi (UNHCR) lilisema kuwa vurugu zinazoendelea kuongezeka katika mkoa wa kusini mashariki mwa Tanganyika nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) zinachochea "maafa ya kibinadamu ya kutisha".
Katika majuma mawili ya kwanza ya mwezi Februari, mashirika yayanayoshirikiana na UNHCR yaliorodhesha matukio 800, ikiwa ni pamoja na mauaji, utekaji nyara na ubakaji. Lakini vurugu nyingi zilifanyika katika maeneo ambayo ni vigumu kwa wafanyakazi wa kibinadamu kufika.