Kasisi wa Kanisa Katoliki nchini DRC aliyetekwa aachiwa huru
Kasisi wa Kanisa Katoliki nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Sebastien Yebo aliyetekwa siku ya Jumamosi na Polisi baada ya kuongoza misa ya asubuhi jana katika Kanisa la Mtakatifu Robert katika eneo la N'sele jijini Kinshasa ameachiliwa huru.
Imechapishwa:
Kasisi Yebo amezungumza na RFI na kuthibitisha kuachiliwa kwake, lakini hakueleza hali ilivyokuwa baada ya kukamatwa.
Walioshuhudia kukamatwa kwake wamesema waliona gari la Polisi likifika katika eneo la Kanisa hilo, na Kasisi huyo kuvamiwa na kupigwa kabla ya watu hao kuondoka naye.
Polisi haijazungumzia tukio hili.
Kanisa Katoliki nchini DRC, imekuwa katika mstari wa mbele kupanga maandamano dhidi ya rais Joseph Kabila, wakimtaka ajiuzulu kuelekea Uchaguzi Mkuu mwezi Desemba.
Baraza la Maaskofu nchini humo wamelaani kukamatwa kwa Kasisi huyo na kusema kuwa halitachoka kuendelea kushinikiza mabadiliko ya kisiasa nchini humo.