Pata taarifa kuu
DRC-USALAMA-SIASA

Jeshi la DRC lashtumiwa kutumia nguvu zaidi kuzima maandamano

Mvutano umezuka nchini DRC kuhusu idadi ya watu waliopoteza maisha wakati wa maandamano yaliyopangwa na Kanisa Katoliki dhidi ya rais Joseph Kabila mwishoni mwa mwaka 2017 kumshinikiza kujiuzulu.

Gari ya polisi ikipiga doria katika mji wa Kinshasa mnamo Novemba 30, 2017, usiku wa kuamkia siku ya maandamano, Desemba 31, 2017.
Gari ya polisi ikipiga doria katika mji wa Kinshasa mnamo Novemba 30, 2017, usiku wa kuamkia siku ya maandamano, Desemba 31, 2017. Junior D. KANNAH / AFP
Matangazo ya kibiashara

Idadi nyingine imetolewa na Umoja wa Mataifa nchini humo MUNUSCO ambayo imeeleza kuwa watu walipoteza maisha ni watano na wengine 120 kukamatwa.

Naye msemaji wa Polisi Kanali Pierrot Mwanamputu amesema ni watu watatu pekee ndio waliopoteza maisha, na kusisitiza kuwa hawakuwa waandamanaji bali watu waliokuwa wanapora mali ya watu.

Aidha, ameongeza kuwa afisa mmoja wa polisi naye aliuawa katika maandamano hayo.

Hii sio mara ya kwanza kwa mvutano kama huu kushuhudiwa wakati kunakuwa na maandamano na kunatokea mauaji katika nchi hiyo ya Afrika ya Kati.

Umoja wa Mataifa, umeitaka serikali ya Kinshasa kuheshimu haki ya kuandamana kwa amani kwa raia wa nchi hiyo.

Mashahidi wanasema watu zaidi ya 140 wakiwemo makasisi walikamatwa na wanaendelea kuzuiliwa katika sehemu mbalimbali nchini DRC.

Huduma ya mtandao wa Internet na SMS imerejea hatua kwa hatua kuanzia jana Jumatatu saa tano usiku (saa za Kinshasa), ambapo wananchi wa taifa hilo tayari wameanza kutumia huduma hiyo iliokatwa tangu siku ya Jumamosi Usiku.

Waziri wa mawasiliano na uchukuzi Emery Okundji amesema serikali ya DR Congo iliyataka mashirika yote yanayotoa huduma hiyo kusitisha huduma hiyo kwa muda, hadi pale watapoamriwa tena kutokana na sababu za usalama wa taifa.

Wakati huo huo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametoa wito kwa rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Joseph Kabila, kuheshimu mkataba wa kisiasa na kukubali kuondoka madarakani.

Wito huu umekuja baada ya kutokea makabiliano kati ya waandamanaji na maafisa wa usalama katika miji mbalimbali nchini humo kushinikiza kujiuzulu kwa rais Joseph Kabila kabange.

Mkataba huo wa kisiasa uliotiwa saini Desemba 31 mwaka 2016, ulimtaka Kabila ambaye amekuwa madarakani tangu mwaka 2001, kuondoka madarakani kufikia Desemba 31 mwaka 2017.

Uchaguzi Mkuu umepangwa kufanyika mwisho wa mwaka huu wa 2018.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.