Jeshi la Nigeria laonywa kuwa makini baada ya shambulio la Boko Haram
Jeshi la Nigeria limeonywa kuchukua tahadhari baada ya magari manne ya jeshi hilo kupotea kufuatia shambulizi lililotekelezwa na kundi la Boko Haram Kaskazini mwa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Taarifa iliyotumwa kwa vikosi vyote vilivyopo kaskazini mwa nchini hiyo, imewataka wanajeshi kuchukua tahadhari baada ya magari hayo maanne kuchukuliwa na kundi la Boko Haram wakati wa makabiliano katika jimbo la Borno.
Katika makabiliano hayo jeshi la Nigeria lilifanikiwa kuwaua wanamgambo tisa wa kundi hilo na kuwajeruhi wengine.
Shirika la habari la AFP limearifu kuwa Jeshi la Nigeria limeamuru mamlaka kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika maeneo ya Maiduguri ili kuyatafuta magari hayo.
Kundi la Boko Haram limekuwa likitumia vifaa vya kijeshi vilivyoibwa kutoka jeshi la Nigeria kutekeleza mashambulizi katika maeneo mbalimbali kaskazini mwa nchi hiyo tangu mwaka 2013.
Maelfu ya watu wamepoteza maisha na mamilioni kuyakimbia makwao kutokana na mashambulizi ya mara kwa mara.