Ouattara akataa mamlaka ya uongozi wa chama chake
Rais wa Cote d'ivoire Alassane Ouattara amejivua mamlaka ya uongozi wa chama tawala cha RDR nchini mwake, hatua ambayo imewashangaza wengi nchini humo.
Imechapishwa:
Ouattara amesema chama hicho kuanzia sasa kitasimamiwa na mwanamama ambaye pia ni mwanasiasa mwenye umaarufu sana katika siasa ya nchi hiyo, bi Henriette Dagri Diabaté, uamuzi ambao umekubaliwa na wanasiasa wengine wa chama hicho, alisema.
Wanasiasa wote wa chama cha RDR walifikiri kuwa katiba mpya ambayo Ouattara aliipitisha mwishoni mwa 2016 ungempa fursa ya kuchukua uongozi wa chama cha RDR, jambo ambalo haliwezekani kutokana na mamlaka ya uongozi wa nchi alio nayo.
"Ni mshangao mkubwa, kwani atakuwa kiongozi wa heshima wa chama cha RDR," alisema Mamadou Touré, mmoja wa makatibu wakuu wa wa chama hicho.
Bw. Ouattara, mwenye umri wa miaka 75, aliyechaguliwa rais wa Côte d'Ivoire mwaka 2010 (alichukua hatamu ya uongozi wa nchini mwaka 2011 kwa sababu ya mgogoro), na alichaguliwa tena mwaka 2015 kwa muhula wa pili na wa mwisho hadi mwaka 2020.
Rais Ouattara alisisitiza kuhusu muungano na chama cha Democratic Party of Ivory Coast (PDCI) cha aliyekuwa rais Henri Konan Bedie katika muungano wa RHDP, hasa kwa lengo la kushinda uchaguzi wa urais wa mwaka 2020. Hasa, alisema anataka ahakikishe vyama hivyo viwe vimejiunga na kuwa chama kimoja kwa muda mfupi.