Pata taarifa kuu
KENYA-SIASA-UPINZANI-AFRIKA

Viongozi wa upinzani barani Afrika wapongeza uamuzi wa Mahakama ya Juu nchini Kenya

Viongozi wa upinzani barani Afrika, wamekuwa wakipongeza hatua ya Mahakama ya Juu nchini Kenya kufuta Uchaguzi wa rais Uhuru Kenyatta wiki iliyopita.

Jaji Mkuu wa Kenya David Maraga (Katikati), rais wa Mahakama ya Juu nchini Kenya
Jaji Mkuu wa Kenya David Maraga (Katikati), rais wa Mahakama ya Juu nchini Kenya REUTERS/Baz Ratner
Matangazo ya kibiashara

Kiongozi wa upinzani nchini Zimbabwe Morgan Tsvangirai, amesema hatua hiyo inaleta matumaini makubwa ya kukua kwa kwa hali ya demokrasia barani Afrika.

Aidha, kiongozi huyo wa chama cha MDC ambaye amewania urais mara tatu dhidi ya rais Robert Mugabe bila mafanikio, ameeleza kuwa ikiwa uamuzi kama huo unaweza kuchukuliwa nchini Kenya, unaweza kufanyika pia nchini Zimbabwe.

Naye kiongozi wa upinzani nchini Burundi Charles Nditije, amesema kilichotokea nchini Kenya ni mfano wa kipekee kwa kuigwa barani Afrika na dunia.

Kiongozi huyo wa CNARED ameongeza kuwa Mahakama ya Juu imeonesha wazi kuwa iko huru na wazi.

Burundi imekuwa katika misukosuko ya kisiasa tangu mwaka 2015 wakati rais Pierre Nkurunziza alipoamua kuwania urais kwa muhula wa tatu kinyume na Katiba na hata kusababisha jaribio la mapinduzi ya kijeshi.

Kiongozi wa upinzani nchini Uganda Kizza Besigye naye ameungana na viongozi wenzake kuipongeza Mahakama ya Juu kwa uamuzi wake.

Besigye ambaye amepambana na rais Yoweri Museveni mara nne bila mafanikio amekuwa akisema kura zake zimeibiwa na aliwahi kwenda Mahakamani kupinga ushindi wa mpinzani wake lakini hakufanikiwa.

Nchini Tanzania mwanasiasa wa chama cha upinzani ACT Zitto Kabwe, amesema uamuzi huo nchini Kenya, nchi yake inabidi iingine haraka kwenye mchakato wa kuibadilisha na kuwa na katiba mpya nchini humo.

Uamuzi huu umesifiwa pia na kiongozi wa upinzani nchini Gabon Jean Ping, ambaye mwaka uliopita, alimtuhumu rais Ali Bongo kumwibia kura.

Naye Cellou Dalein Diallo kiongozi wa upinzani nchini Guinea, amesema kilichotokea nchini Kenya kinatia moyo sana kwa maendeleo ya demokrasia nchini humo.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.