CENI kuchapisha "kalenda ya kupiga kura" hivi karibuni DRC
Mwenyekiti wa tume ya uchaguzi nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Corneille Nangaa amesema kalenda ya Uchaguzi mkuu itatangazwa hivi karibuni.
Imechapishwa:
Kauli hii imekuja siku moja baada ya tume hiyo kutangaza kuwa jumla ya wapiga kura milioni 40 wameandikishwa kwenye majimbo 24 na kwamba kuanzia tarehe nne itaanza kuwaandika wapiga kura kwenye majimbo mawili ya Kasai.
Serikali ya Kinshasa imesema zoezi la kuwaandika wapiga kura litaanza kukamilika kabla ya kutangaza mambo mengine.
Mapema wiki hii Tume ya taifa ya Uchaguzi nchini DRC (CENI) imesema zoezi la kuhakiki na kuandikisha wapiga kura wapya kwenye majimbo mawili ya Kasai ambako kumeshuhudiwa machafuko hivi karibuni, litaanza September 4 na kisha kuendelea kwenye majimbo mengine 24
Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi CENI, Corneille Nangaa aliwataka wananchi kuwasaidia maofisa wake kufanya kazi kwa uhuru kuandaa uchaguzi.
Katika hatua nyingine upinzani umekosoa takwimu za hivi karibuni zilitolewa na tume hiyo ukisema kwamba kiwango kikubwa hakiko sawa.
CENI ilisema jumla ya wapiga kura milioni 40 wameandikishwa kwenye majimbo mengine 24 huku taifa hilo likiwa na jumla ya raia milioni 70 wengi wakiwa bado hawajaandikishwa.