Jeshi la DRC lasema linadhibiti mji wa Kipese baada ya kuwashinda waasi
Jeshi la Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo FARDC limetangaza kuurejesha kwenye himaya yake mji wa Kipese Mashariki mwa nchi hiyo baada ya waasi Mai Mai kuudhibiti kwa muda wa siku moja.
Imechapishwa:
Kundi la waasi la Mai-Mai Mazembe liliuteka mji huo mwishoni mwa wiki iliyopita.
Mji huo unategemewa kiuchumi pamoja na ule wa Butembo, ambao pia upo katika njia ya kuingilia kuelekea Lubero katika mkoa wa Kivu Kaskazini.
Kwa mujibu wa msemaji wa jeshi la FARDC Jules Tshkudi, wanajeshi wawili wamepoteza maisha kufuatia majeraha walioyapata wakati wa mapambano huku waasi watano wakiuawa.
Tangu mwezi Juni mwaka huu, makundi ya Mai Mai yamekuwa yakijaribu kudhibiti maeneo muhimu ya Mashariki mwa nchi hiyo.
Mafanikio haya yamekuja baada ya mwanahabari wa Marekani Lisa Dupuy aliyekuwa ametekwa jimboni Ituri kuachiwa huru.