Cyril Ramaphosa kuzuru Lesotho kabla ya uchaguzi
Mratibu wa mazungumzo ya kisiasa nchini Lesotho kutoka Jumuiya ya maendeleo ya nchi za kusini za Afrika, SADC, ambaye pia ni makamu wa rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa, Jumanne hii anazuru nchi hiyo inayojiandaa kwa uchaguzi mkuu mwezi Juni mwaka huu.
Imechapishwa:
Cyril Ramaphosa na kamati ya usuluhishi ya SADC walipewa mamlaka na wakuu wa nchi hizo kufanya mazungumzo ya kitaifa nchini Lesotho kabla ya kufanyika kwa uchaguzi mkuu, zoezi ambalo wakuu hao wa nchi walitaka zoezi hili lifanyika kabla ya uchaguzi mkuu.
Kwa mara ya kwanza Ramaphosa alienda nchini Lesotho mwaka 2014 na toka wakati huo kila mara anaporejea nchini humo kumekuwa na mjadala mkali ikiwa upatanishi wake umefanikiwa kutuliza joto la kisiasa nchini humo.
Mashirika ya kiraia nchini Lesotho yameeleza kusikitishwa na namna makamu wa rais wa Afrika Kusini anavyoratibu zoezi la upatanishi wa kisiasa nchini Lesotho, yakisema muda anaotumia nchini humo ni mdogo kuliko matatizo yaliyopo.
Huu utakuwa ni uchaguzi wa tatu kufanyika nchini Lesotho katika kipindi cha miaka mitano.