Upinzani nchini Zambia wamtuhumu rais Lungu kupanga kukamatwa kwa kiongozi wao
Chama cha upinzani nchini Zambia UPND, kinataka kuachiliwa huru kwa kiongozi wao Hakainde Hichilema ambaye amezuiwa baada ya kufunguliwa mashitaka ya uhaini, wakimshutumu rais Edgar Lungu kwa kuhusika na kukamatwa kwa kiongozi wao.
Imechapishwa:
Viongozi wa chama hicho wameishtumu serikali kwa kumhangaisha kiongozi wao kuanzia mwaka uliopita wakati wa kipindi cha Uchaguzi Mkuu.
Hatua hii imekuja baada ya mwanasiasa huyo kukamatwa Jumanne asubuhi kwa madai kuwa alizuia msafara wa rais Edgar Lungu mwishoni mwa wiki iliyopita.
Hichilema alikamatwa siku ya Jumanne na kufikishwa katika kituo cha polisi jijini Lusaka kwa madai kuwa alizuia kupita kwa msafara wa rais Lungu mwishoni mwa wiki iliyopita.
Polisi wanasema kitendo hicho cha mwanasiasa huyo kilihatarisha maisha ya rais Lungu.
Kupitia ukurasa wake wa Twitter, kiongozi huyo wa upinzani alidai kuwa rais Lungu anataka kumuua.
Geoffrey Bwalya Mwamba, Naibu rais wa chama cha UPND akizungumza na wanahabari jijini Lusaka siku ya Alhamisi, ameshutumu kukamatwa kwa kiongozi wao na kushutumu maafisa wa polisi kwa kushindwa kumudu msafara wa rais Lungu, na hivyo wanataka kujiuzulu kwa Inspekta Mkuu wa Polisi nchini humo.
Aidha, Mwamba amesema mashitaka dhidi ya Hichilema yamechochewa kisiasa na kuongeza kuwa polisi wamepanga kumkamata wakati wowote.
Mwamba ambaye alikuwa katika msafara na Hichilema, amesema alikuwepo kwenye msafara huo na hawakuwahi kuzuia msafara wa rais Lungu.
Kiongozi huyo wa upinzani anatarajiwa kufikishwa Mahakamani siku ya Jumanne wiki ijayo.
Hichilema alikabiliana na rais Lungu katika Uchaguzi wa urais mwaka uliopita, zoezi ambalo upinzani umekuwa ukisema kuwa halikuwa huru na haki.