Upinzani nchini DRC waitisha maandamano kupinga uteuzi wa Waziri Mkuu Bruno Tshibala
Muungano wa vyama vya upinzani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo umeitisha maandamano ya nchi nzima, kupinga uteuzi wa Bruno Tshibala kuwa Waziri Mkuu mpya.
Imechapishwa:
Wanasiasa wa Rassemblement wanasema kuwa hawatambui uteuzi wa Tshibala ambaye alijondoa katika upinzani baada ya mazungumzo ya kisiasa.
Upinzani nchini DRC unasema uteuzi huu uliofanywa na rais Joseph Kabila wiki iliyopita, ni mbinu ya kiongozi huyo kuendelea kukaa madarakani na kuchelewesha utekelezwaji wa serikai ya mpito kuelekea Uchaguzi Mkuu.
Uteuzi wa Tshibala ambaye ameomba kuungwa mkono na kila mmoja, ulikuja baada ya rais Kabila kulihotubia bunge na kuahidi kumteua Waziri Mkuu baada ya saa 48.
Kumekuwepo na mvutano mkali kati ya upinzani wa Rassemblement, serikali na wapinzani wengine kuhusu ni nani awe Waziri Mkuu.
Rassemblement wamekuwa wakitaka Felix Tshisekedi kuwa Waziri Mkuu, huku wapinzani wengine wakipinga pendekezo hilo.
Mvutano huu wa kisiasa nchini humo umeshutumiwa pia na Umoja wa Ulaya licha ya mkataba kupatikana mwaka uliopita.
Wiki iliyopita, kulikuwa na mgomo wa nchi nzima, kushinikiza serikali kutekeleza mkataba huo kikamilifu.
Mkataba huo wa kisiasa unataka kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu mwisho wa mwaka huu lakini hadi sasa haijafahimika ikiwa hilo litatimia.
Ni mvutano ambao pia umeendelea kuchelewesha mazishi ya Ettiene Tshisekedi aliyekuwa kiongozi wa muungano wa upinzani aliyefariki dunia mwezi Februari nchini Ubelgiji.