Burkina Faso: Kundi la kiislamu lakiri kuhusika kwenye shambulio dhidi ya vituo 2 vya polisi
Wanajihadi wa kiislamu wamekiri kuhusika katika shambulio la usiku wa kuamkia Jumanne Februari 28, shambulio lililolenga vituo viwili vya polisi nchini Burkina Faso, ambapo pia walihusika na mauaji ya wanajeshi 12 kwenye shambulio la mwezi Desemba mwaka jana.
Imechapishwa:
Mamlaka nchini Burkina Faso zinasema kuwa hakuna vifo vyovyote vilivyotokana na shambulio hilo, lakini zikathibitisha kuwa mwanamke mmoja polisi alijeruhiwa, amesema afisa wa juu wa Serikali kwenye mji ambao lilitekelezwa shambulio hilo kwenye mpaka na Mali.
Shambulio hili limetekelezwa wakati huu mjini Ouagadougou kukiendelea tamasha la kimataifa la filamu, ambako nako usalama umeimarishwa maradufu.
Kwa mujibu wa Mohamed Dah kiongozi wa kijiji ambako shambulio hili limetekelezwa, amesema kuwa washambuliaji walikuwa kwenye pikipiki ambapo baada ya kufika kwenye vituo hivyo walianza kufyatua risasi hovyo kulenga vituo hivyo vya polisi.
Kundi la Ansarul Islam lilikiri kuhusika kwenye shambulio la Desemba 16 mwaka jana, ambapo wanajeshi kadhaa waliuawa jirani na mpaka na nci ya Mali, hili likiwa shambulio baya zaidi kuwalenga wanajeshi.
Wataalamu wanasema kundi hilo linaongozwa na muhubiri Malam Ibrahim Dicko ambaye anataka kuanzishwa kwa utawala wa kiislamu kwenye eneo hilo.
Mashambulizi mengi ya makundi ya kiislamu yamekuwa yakitekelezwa kaskazini mwa nhci hiyo kwenye mpaka na nchi ya Mali, lakini Januari 30 mwaka 2016 watu zaidi ya 17 waliuawa kwenye shambulio la mjini Ouagadougou ambapo washambuliaji walivamia migahawa na hoteli za kitalii.